Header Ads

Jitihada za Dkt. Shein zamletea pongezi kutoka ‘Help Age International’

Shirika la Kuwahudumia Wazee Duniani ‘Help Age International’ limetoa pongezi maalum kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kutokana na juhudi alizozichukua na kuziendeleza za kuwatunza vyema wazee hapa nchini hasa kwa kuanzisha ‘Pencheni Jamii.
Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Kuwahudumia Wazee Duniani ‘Help Age International’ Arun Maira akiwa na ujumbe wake kutoka Shirika hilo aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazugumzo na Rais Dk. Shein Ikulu mjini Zanzibar.
Arun Maura alieleza kuwa Mpango uliochukuliwa na Dk. Shein wa kuanzisha ‘Pencheni jamii’, kwa wazee waliofikia umri wa miaka 70, bila ya kujali historia ya kazi walizokuwa wakifanya ni jambo ambalo limeipa sifa kubwa Zanzibar Kitaifa na Kimataifa.
Alieleza kuwa katika ziara yake hapa Zanzibar alivutiwa sana na ubunifu unaoendelezwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuzishirikisha taasisi mbali mbali za Serikali katika kuwalinda, kuwatunza na kuwaendeleza wazee hapa nchini.
Alisema kwamba hali hiyo ni tofauti na nchi nyingi ambazo suala hilo hufanywa na taasisi moja peke yake jambo ambalo hupelekea ugumu wa kutatua changamoto mbali mbali zinazowakabili wazee katika maisha yao.
“Kwa hatua hii , Rais Dk. Shein, Shirika hili linakupongeza sana tena sana kwani kazi kubwa umeifanya wewe na Serikali yako katika suala zima la kuwaenzi wazee, kuwatunza na kuwaendeleza na tayari nchi nyingi zimeona choyo cha kimaendeleo na zinataka kuja kuiga mfumo huu…hongera sana:”alisema Arua Maura.
Aidha, alieleza kwamba licha ya kuwepo nchi nyingi zilizokuwa na uwezo mkubwa wa kiuchumi katika Bara la Afrika na duniani kwa jumla lakini bado hazijaweza kuanzisha utoaji wa Pencheni kama hiyo kwa wazee wa nchi zao.
Mwenyekiti huyo aliongeza kuwa hivi sasa ziko nchi mbali mbali zinataka kuja kujifunza Zanzibar kutokana na mafanikio yalipatikana baada ya kuanzisha ‘Pencheni Jamii’ hasa baada ya kupata taarifa kupititia vyombo mbali mbali vya habari duniani ambavyo vimekuwa vikiitangaza Zanzibar kutokana na mafanikio hayo.
Nae Rais Dk. Shein kwa upande wake alieleza kufurahishwa kwake kwa kupata salamu na pongezi hizo na kuona kwamba nchi nyingi zimevutiwa na utaratibu uliozishwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwajali wazee.
Hata hivyo, alieleza kwamba juhudi anazoendelea kuchukua hivi sasa za kuwatunza, kuwalinda na kuwaendeleza wazee ni mwendelezo wa fikra na mawazo ya muwasisi wa Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume ambaye alibuni na kuazisha mipango na taratibu mbali mbali za kuwatunza wazee ikiwa ni pamoja na kuanzisha nyumba za wazee Unguja na Pemba.
Hivyo Dk. Shein alieleza kuwa atahakikisha kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya Saba inaendeleza fikra na mfumo huo kwa nguvu zake zote hasa ikizingatiwa kwamba wazee wanamchango mkubwa katika maendeleo yaliofikiwa hivi sasa katika Taifa hili.
Dk. Shein alieleza kuwa wazee ni hazina kubwa hapa nchini na kuahidi kuwa Serikali anayoiongoza itahakikisha inaendelea kuwaunga mkono wazee kwa mashirikiano ya pamoja na Mashirika mbali mbali ya ndani na nje ya nchi.
Pamoja na hayo, Dk. Shein alitoa pongezi maalum kwa Shirika hilo linalowahudumia wazee Duniani kwa juhudi zake inazoziendeleza katika kuiunga mkono Zanzibar katika suala zima la kuimarisha ustawi wa wazee kwa kipindi kirefu tokea kuanzishwa kwake.
Aidha, Dk. Shein alilipongeza Shirika hilo kwa kuendelea kushirikiana na nchi mbali mbali duniani katika kuwaenzi na kuwatunza wazee.
Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza kwamba itakuwa ni vyema kwa ofisi hiyo kuimarisha ofisi zake hapa Zanzibar hatua ambayo itaisaidia Serikali kufanya kazi kwa karibu na Shirika hilo katika kulinda ustawi wa wazee.

No comments