Header Ads

Shamata: Tunajenga haya Matawi kuimarisha CCM yetu



MWAKILISHI wa jimbo la Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba, Mhe. Shamata Shaame Khamis amewahakikishia wanachama wa Chama cha Mapinduzi –CCM- kuendelea kushirikiana na viongozi mbalimbali wa matawi katika utekelezaji wa majukumu ya Chama ikiwemo upatikanaji wa Ofisi za Chama katika kila Tawi jimboni kwake.

Kauli hiyo ameitoa wakati akizungumza na vijana mara baada ya kukamilika kwa zoezi la uwekaji wa kifusi katika Ofisi ya CCM Tawi la Maziwang’ombe inayojengwa kupitia juhudi za mwakilishi huyo.
Mwakilishi wa jimbo la Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba, Mhe. Shamata Shaame Khamis akishiriki zoezi la utoaji wa Kifusi katika Jengo la Ofisi ya CCM Tawi la Maziwang’ombe.
 Khamis amesema kuwa, lengo la ujenzi wa ofisi za CCM katika Matawi yake ni kuhakikisha inaendelea kuwatumikia wananchi kwa ukaribu, ikiwa ni pamoja na kuongeza idadi ya wanachama zaidi.

“lengo la kutengeneza matawi si kwamba chama kinakuwa kinatengeneza fedha, bali kazi yake kubwa ni kuhakikisha CCM inaendelea kushinda katika chaguzi mbalimbali na huu ndio mtaji wetu,” alisema Mwakilishi huyo.

Katika hatua nyingine mwakilishi huyo aliendelea kuwasisitiza vijana kujiepusha na vitendo vya utumiaji wa Dawa za kulevya kwani Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haipo tayari kuona vitendo kama hivyo vinaendelea kujitokeza ndani ya wilaya hiyo.

“Tunaona juhudi kubwa zinazoendelea kuchukuliwa na Uongozi wa Wilaya yetu chini ya Mkuu wa Wilaya, Salama Mbarouk Khatib wa kupambana na Dawa za kulevya pamoja na Pombe haramu, hivyo basi nakuombeni sana jiepusheni kujiingiza katika masuala haya kwani endapo utagundulika hatua kali zitachukuliwa dhidi yako,” alisema Shamata.
Katibu wa Tawi, Khatib Said Juma akimwelezea Mwakilishi Shamata kuhusu ujenzi wa Afisi za Tawi hilo
Katibu wa Tawi hilo, Khatib Said Juma amewapongeza vijana kwa kuendelea kuwa na moyo wa kujitolea na kuwataka kuendelea kutoa mashirikiano kwa viongozi wao ili kuona kwamba maendeleo yanapatikana kwa haraka zaidi.

“Niwashukuruni sana vijana kwa kazi mliyoifanya leo, na nawaombeni muendeleze mashirikiano haya baina ya viongozi wetu wa Chama na Serikali ikiwa ni pamoja na kuendelea kudumisha Amani katika maeneo yetu,” alisema Juma.
Mwenyekiti wa UVCCM wa Tawi hilo, Juma Mbarouk Khamis, akimkaribisha Mwakilishi huyo kuzungumza na Vijana mara baada ya Zoezi la uwekaji wa Fusi katika Jengo hilo kukamilika. (PICHA ZOTE NA GASPARY CHARLES- MICHEWENI REDIO)
Awali Mwenyekiti wa UVCCM wa Tawi hilo, Juma Mbarouk Khamis, akimkaribisha Mwakilishi huyo katika Zoezi hilo, alimuahidi Mwakilishi kwamba Vijana wa Tawi la Maziwang’ombe wataendelea na juhudi zao za kukitumikia pamoja na kukilinda Chama hicho ili kiendelee kuaminika zaidi kwa wananchi wake.

“Ndugu Mheshimiwa, naomba tukuhakikishie tu kwamba, sisi vijana wa Tawi hili la Maziwang’ombe tupo tayari kuendelea kutoa nguvu zetu kwa vyovyote vile ili kuhakikisha CCM inaendelea kuaminika kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kuendelea kushinda katika chaguzi zote, na ndiomana tumeamua kuungana pamoja hapa kuhakikisha tunafanikiwa ujenzi wa Tawi hili,” alisema Mwenyekiti huyo.

Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Tawi la CCM katika Wadi ya Kiuyu-Maziwang’ombe Wilaya ya Micheweni, ni moja ya juhudi za Mwakilishi wa Jimbo hilo Mhe. Shamata Shaame Khamis, za kutaka kuimarisha nguvu za Matawi kwa kuwa na Ofisi zake, ambapo jengo hilo linatarajiwa kukamilika ifikapo mwishoni mwa Mwaka 2018.

No comments